Tafiti Mpya ya George Lohay Imechapishwa

Kichwa cha Tafiti: Ushahidi wa Jenetiki wa kugawanyika kwa idadi ya Twiga wa Masai waliotenganishwa na Bonde la Gregory nchini Tanzania (linki)

Mshiriki mpya wa timu ya RISE, George Lohay, tayari ameanza kujenga njia mpya na kufanya maendeleo ya kuhifadhi wanyamapori wa Afrika. George amekuwa na sababu nyingi za kusherehekea hivi karibuni – alijiunga na RISE kama Mtafiti wa Sayansi katikati ya mwezi Mei, na hivi karibuni, utafiti wake kuhusu kugawanyika kwa jenetiki za twiga wa Masai ulichapishwa katika jarida maarufu la Ecology and Evolution.

Kuanzia mwaka 2019, George na kikosi cha watafiti kutoka Chuo Kikuu cha Penn State walichunguza muundo wa jenetiki wa jamii za twiga wa Masai katika mfumo wa ikolojia ya Serengeti na Tarangire. Mazingira haya mawili yako tofauti kijiografia na Bonde la Gregory la Tanzania linawatenganisha, na utafiti wao ulichunguza kivipi na jinsi jamii za twiga zinavyoingiliana.

Juhudi za utafiti zilijibu, kwa sehemu, wasiwasi unaoongezeka kuhusu kupungua kwa idadi ya twiga ulimwenguni. Kwa ongezeko la uwindaji haramu na uharibifu wa mazingira  unaotokana na makazi na miundombinu ya binadamu, spishi inayojulikana sana katika mandhari hii inaanza kupungua. Kwa kweli, katika miaka 30 iliyopita pekee, inakadiriwa kuwa idadi ya twiga wa Masai – spishi ya asili ya kusini mwa Kenya na Tanzania ambayo hapo awali ilikuwa na idadi ya takriban 70,000 – imepungua kwa asilimia takriban 50, na hivyo kuwapelekea kuingia kwenye orodha ya IUCN ya spishi zilizoko kwenye hali hatarishi mwaka 2019 (Lohay et al., 2023).

Alipoulizwa kuhusu chanzo cha msukumo wa utafiti wake, George alieleza kwamba kupungua kwa kiasi kikubwa kwa twiga wa Masai kunamaanisha kwamba spishi hii ni nyeti sana, na ili kuwalinda vizuri, tunahitaji kuelewa mambo mengi yanayowaathiri haraka iwezekanavyo. George alijua mara moja maswali aliyotaka kuchunguza kuhusu twiga wa Masai, hasa kwa sababu alikamilisha utafiti kama huo kuhusu idadi ya tembo mwaka 2018 kama sehemu ya PhD yake. Aidha, George alitaja kwamba daima amekuwa na upendo binafsi kwa twiga: “Ni wanyama wenye utulivu sana… wanawasiliana sana wao kwa wao, na wanajenga urafiki wa muda mrefu ambao baadhi ya watu wanadhani unaweza kudumu kwa maisha yao yote. Hilo daima lilinifanya nipendezwe nao sana.”

Kujibu wito wa kimataifa wa kuelewa spishi hii hatarishi vyema, George na timu yake  walikwenda Tanzania mara tatu kwa nyakati tofauti, kila mara kwa kipindi cha miezi miwili hadi mitatu. Walipofika kwenye maeneo ya tafiti, watafiti walianza mchakato wao wa ukusanyaji wa data; waliwafuatilia twiga wa Masai, kusubiri kwa uvumilivu asili ifuate mkondo wake, na hatimaye kukusanya sampuli za kinyesi cha twiga kwa ajili ya uchambuzi. Mwaka 2021, timu iligundua kwamba utafiti unaweza kunufaika kutokana na sampuli za tishu za twiga mbali na sampuli za kinyesi, na wakati huo walianza kufanya kazi na Daktari wa wanyama kutoka Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori Tanzania ili kukusanya sampuli ndogo kwa ajili ya utafiti kwa usalama.

Dkt. George Lohay na Emmanuel Kimaro wanakusanya sampuli za kinyesi cha twiga. (Picha: James Madeli)

Hatimaye, utafiti ulionyesha kwamba twiga wanakabiliwa na hatari zaidi kuliko ilivyodhaniwa awali. George na timu yake waligundua kwamba jamii hizo mbili hazijakuwa zikishirikiana au kuchanganyika kimahusiano, hivyo kusababisha kuwepo kwa jamii mbili tofauti kijenetiki. Walikadiria kwamba twiga wa kike hawajahamia Bonde la Ufa kutoka ikolojia moja hadi nyingine kwa miaka 289,000 iliyopita, na twiga wa kiume hawajahamia kwa angalau maelfu ya miaka ya hivi karibuni. Twiga wa Masai waligundulika kukabiliana na vipande vya asili vya makazi kutokana na milima migumu ya Bonde la Ufa, pamoja na kuingiliwa na binadamu katika makazi ya wanyama porini. Kwa bahati mbaya, aina hii ya kugawanyika kwa mazingira inaweza kuonekana katika sehemu kubwa ya Afrika Mashariki, kwani maeneo ya makazi ya wanyama porini yanabadilishwa zaidi kwa matumizi mengine ili kuunga mkono ongezeko la idadi ya watu.

Uhamiaji na kuchanganyika kwa uzao ni muhimu kwa kujenga uthabiti wa mazingira kwa sababu husaidia katika kukuza aina mbalimbali za kijenetiki, hivyo kupunguza hatari za magonjwa, mabadiliko ya kijenetiki, na vitisho vingine (McCormick, 2023). Kwa kuzingatia hilo, utafiti uligundua ishara za uingiliano wa uzao kwa kila jamii, mtiririko ambao unapunguza utofauti wa kijenetiki na afya ya jamii za wanyama porini. Uvumbuzi huu unaimarisha zaidi umuhimu wa utafiti huu na dharura ya kuhitajika kwa juhudi mpya za uhifadhi.

Kuonyesha umuhimu wa kuendeleza suluhisho za uhifadhi zenye ubunifu na zenye ufanisi kwa kila moja ya jamii hizi tofauti, George alielezea: “[Matokeo haya] ni muhimu kwa sababu sasa tunahitaji kufikiria kuhusu twiga wa Masai kama kitengo muhimu cha mageuzi. Badala ya kufikiria kuhusu twiga 35,000 wanaobaki porini, tunafikiria kwamba kila kitengo ni muhimu peke yake na kitahitaji juhudi maalum zilizobinafsishwa kwa kila kitengo cha jamii ili kuzihifadhi kwa kuwa kwa asili hazifanani.” George pia alisisitiza umuhimu wa korido za wanyama porini katika mabadiliko ya idadi ya jamii hizi, akisisitiza kuwa bila uhifadhi, korido chache za wanyama zilizosalia zitafungwa kabisa, hivyo kuunda vizuizi vya ziada kwa wanyama pori.

Kwa siku za usoni, George anatumaini kuona twiga wakilindwa na kueleweka vyema. George na washirika wake kutoka Taasisi ya Wild Nature na Chuo Kikuu cha Penn State tayari wamechukua hatua kuelekea utafiti mpya kuhusu uunganishaji kati ya jamii za twiga katika maeneo ya Kaskazini na Kusini mwa Tanzania. Anatumaini kuona watafiti zaidi, hasa vijana, wakitumia zana za kijenetiki katika utafiti: “Kwa kutumia zana za kijenetiki, tunaweza kutoa habari kwa taasisi za uhifadhi au serikali kuhusu uunganishaji ambao unaweza kusaidia kuunda sera za kulinda wanyama hawa kwa muda mrefu. Nadhani tunahitaji kuendelea kuhamasisha vijana wetu kushiriki katika utafiti kwa sababu inahitaji miaka mingi na itatoa habari kwa wale wanaofanya maamuzi.”

Kwa kukusanya watafiti wenye hamasa kama George, ambao hutumia utafiti kama njia ya kuhimiza na kuboresha uhifadhi, tunatumaini kwamba spishi hii maarufu na nyingine kama hii zitapata nafasi ya kuongozeka tena siku zijazo.

George anatoa shukrani kubwa kwa timu ya utafiti iliyoshirikiana naye kukamilisha utafiti huu. Hasa, George alishirikiana na wachunguzi wakuu: Derek Lee, Profesa Msaidizi wa Utafiti wa Baiolojia katika Chuo Kikuu cha Penn State na Mwanasayansi Mkuu wa Taasisi ya Wild Nature, na Douglas Cavener, Profesa wa Baiolojia katika Chuo Kikuu cha Penn State. Aidha, alitaja mchango mkubwa wa Monica Bond, Mwanasayansi Mkuu wa Taasisi ya Wild Nature, pamoja na watafiti wengine kutoka Chuo Kikuu cha Penn State, Lan Wu-Cavener, David L. Pearce, na Xiaoyi Hou.

Kuchangia programu za utafiti wa vitendo vya GF, bonyeza hapa.

                  

Tafadhali tambua kuwa unahamishwa kwenda kwenye kurasa ya Shirika la Uhifadhi na Jamii za Kiafrika, Inc.

Nchini Marekani, Grumeti Fund ni mradi unaosaidiwa-kifedha na Shirika la Uhifadhi na jamii za Kiafrika, Inc. (“ACCF”), shirika la kimsaada 501(c) (3). Michango yenye kutozwa kodi kwa ACCF hutolowa kwa Grumeti Fund kusaidia kazi yetu.

Bonyeza hapa kuchangia